Rai imetolewa kwa viongozi mbalimbali kufanya kazi kwa ushirikiano na maelewano lengo ikiwa ni kuhakikisha kunakuwa na uongozi wa pamoja wenye kuleta maendeleo ambapo imebainishwa kuwa changamoto nyingi huanzia katika ngazi ya kijiji hivyo ni vema kila mmoja akabadilika katika utendaji wake wa kazi badala ya kutumia madaraka yao kinyume na inavyostahiki ili kutoleta migogoro.
Mkuu wa wilaya ya Kilosa Alhaji Majid Mwanga ametoa rai hiyo Julai 19 mwaka huu wakati wa kikao cha kamati ya uvunaji wa misitu ambapo amesema uongozi wa pamoja ni kitu cha muhimu kwani utendaji wa Serikali unahitaji kila mmoja kumtambua kiongozi mwenzake kama sehemu yake ya kazi kwani kwa kufanya hivyo itasaidia kazi kufanyika katika utaratibu mzuri na ushirikiano huku akisisitiza taratibu za kiutendaji kufuatwa kwa mujibu wa taratibu,sheria na kanuni huku akitaka kufuatwa kwa taratibu za kila sekta kama zinavyoelekeza ikiwemo kutotumika vibaya kwa madaraka waliyonayo ambapo ametaka maafisa tarafa, watendaji wa kata, watendaji wa vijiji na wenyeviti wa vijiji pamoja na wataalam kufanya kazi kwa kuheshimiana jambo litakalosaidia kuwa na timu moja yenye mtazamo chanya wa kuleta maendeleo.
Afisa Maliasili Mkoa John Chuwa
Mhifadhi Misitu Mkuu Wilaya Samwel Nyabange
Kwa upande wake Afisa Maliasili Mkoa Joseph Chuwa amewataka viongozi wa vijiji kutojihusisha na uvunaji haramu ambapo pia amesisitiza usimamizi shirikishi na uvunaji endelevu ambapo pia ametaka kuwepo kwa umakini kwa majina yanayopitishwa kwa kuzingatia zaidi taratibu zinavyoelekeza sambamba na kuweka rekodi na kumbukumbu kwani kumekuwa na hulka ya baadhi ya waombaji kuomba maeneo lakini hawayafanyii kazi jambo linalosababisha upotevu wa mapato huku Mhifadhi Misitu Mkuu Wilaya Samwel Nyabange akibainisha sababu zilizopelekea kutofikia malengo ya makusanyo ya fedha ikiwemo mabadiliko ya bei ya mazao ya misitu mwaka 2020, kuongezeka kwa mahitaji ya mbao pandwa katika soko, miundombinu mibovu ya barabara hasa kipindi cha masika, uwepo wa wimbi la ugonjwa wa COVID 19, uchache wa watumishi na vitendea kazi, uwepo wa njia nyingi za utoroshaji wa mazao ya misitu migogoro ya mipaka kati ya Wilaya na Wilaya, vijiji na vijiji.
Katika kuhakikisha udhibiti wa misitu unafanyika ipasavyo Kamanda wa TAKUKURU Wilaya Gwakisa Mwaikela amesema zipo namna mbalimbali za kufanya udhibiti ili kutopoteza mapato ikiwemo kuhakikisha magogo yote yanayovunwa yanagongwa muhuri eneo husika la kuvunia ikiwemo kudhibiti wavunaji wote wasiovuna maeneo stahiki waliyoomba ama kuvuna kiasi pungufu ya walichoomba sambamba na kuwadhibiti kwa kutowapa leseni ama kibali kwa mara nyingine endapo hawatavuna kwa mujibu wa makubaliano ambapo pia ameshauri kutoruhusiwa kwa mvunaji yoyote pasipokuwa na risiti ya ushuru wa kijiji inayomruhusu kuvuna baada ya kulipia jambo litakalosaidia vijiji na Halmashauri kuingiza mapato.
Akieleza taarifa ya upandaji miti Afisa Maliasili Wilaya John Mtimbanjai amesema ili kukabiliana na changamoto ya kutoweka kwa rasilimali ya Misitu, jamii inahamasishwa kupanda miti katika maeneo wanayoishi, maeneo ya taasisi na maeneo ya mashamba binafsi ya wananchi huku upande wa mikakati iliyopo kuzuia uharibifu wa misitu hii ni pamoja na kuendelea kutenga bajeti na kushirikiana na wadau kuwezesha Mipango ya Matumizi bora ya ardhi ya vijiji, kuainisha mipaka ya misitu ya hifadhi za serikali kuu, halmashauri na vijiji kwa kuweka beacons/alama na kufyekea barabara ya mipaka inayotenga hifadhi na maeneo ya vijiji, kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa misitu hii kwa ustawi na maendeleo ya jamii, kufanya doria za mara kwa mara ndani na nje ya misitu ili kudhibiti uharibifu, kushirikisha kamati za maliasili za vijiji na jamii kwa ujumla katika kulinda rasilimali za nchi, kuanzisha bustani za miti vijijini ili kupanda miti katika maeneo yaliyoharibiwa na pia kugawa miche kwa wananchi ili wapande katika maeneo yao, kusisitiza kufuata sheria na taratibu za kupata vibali kabla ya kufyeka misitu au kukata miti, kuchukua hatua kwa wanaokiuka taratibu za kuvuna au kukata miti na kufanya ufuatiliali hali ya uvunaji katika vijiji vinavyovuna mazao ya misitu.
Halmashauri ya Wilaya Kilosa
Sanduku la posta: S.L.P 65 Kilosa
Simu: 023 2623093
Simu: 0756468146
Barua Pepe: ded@kilosadc.go.tz
Hatimiliki imehifadhiwa ©2017 Halmashauri ya Wilaya Kilosa