Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Sanaa, Utamaduni na Michezo na ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa amezitaka Tawala za Mikoa, Halmashauri na Taasisi zilizo chini ya TAMISEMI kuzingatia maelekezo ya Rais Samia kuwa vitengo vya mawasiliano serikalini viimarishwe kwa kupatiwa vitendea kazi kama vile Kamera, Kompyuta n.k ili kutekeleza majukumu yao kiufasaha kwa kufanya mawasiliano ya kimkakati lengo ikiwa kutekeleza azma na maono ya Serikali ya awamu ya sita.
Msigwa ametoa rai Mei 25, 2025 wakati akifunga kikao kazi cha siku mbili cha Maafisa habari wa tawala za mikoa, halmashauri na taasisi zilizo chini ya TAMISEMI, kilichofanyika tarehe 23.05.2025 na 24.05.2025 katika ukumbi wa Jiji la Dodoma mji wa Serikali Mtumba.
Katibu Mkuu huyo amekemea kasumba ya baadhi ya Viongozi wa Halmashauri wanaodhani vitengo vya Mawasiliano Serikalini havihitaji fedha. Amesema katika mwaka huu wa uchaguzi mkuu viongozi hao wahakikishe Maafisa habari wanawezeshwa fedha na kwenda kwenye vyombo vya habari kueleza mazuri ambayo serikali imeyatekeleza katika maeneo yao.
"Nakuomba tukafanye kazi zetu kimkakati ili kufikia malengo ya serikali na taasisi mnazofanyia kazi" amesema Msigwa.
Katika hatua nyingine, Msigwa amewajulisha maafisa habari jukumu jipya la usimamizi na uratibu wa masuala ya mitandao ya kijamii ambalo Idara ya Habari Maelezo imekabidhiwa na kuwataka maafisa husika wenye changamoto katika eneo hilo wawasiliane na habari maelezo ili kupata msaada na kuzilinda akaunti za social media za taasisi zao dhidi ya watu wenye nia ovu.
Halmashauri ya Wilaya Kilosa
Sanduku la posta: S.L.P 65 Kilosa
Simu: 023 2623093
Simu: 0737847880
Barua Pepe: ded@kilosadc.go.tz
Hatimiliki imehifadhiwa ©2017 Halmashauri ya Wilaya Kilosa